Thursday, 22 January 2015

PLUIJM UMEJIANDAA NA MECHI YA SIMBA?



Na Ramadhani Ngoda
Waswahili husema, “mazoea hujenga tabia”. Na hii ndio inayoonekana katika soka letu kwa sasa ambapo ambapo mambo madogo madogo hukomaa na kuwa tabia za vilabu vyetu hapa nchini jambo ambalo linapeleka soka la nchi hii kusiko.
Ni wazi sasa kauli ya kiingereza inayosema “they are hired to be fired” inayotafsirika “wanaajiriwa ili watimuliwe” inaonekana kuthibitika zaidi ktika soka.
Kutimuliwa kwa kocha wa Yanga Marcio Maximo ambaye pia aliwahi kuwa kocha wa timu ya taifa ya Tanzania baada ya mchezo dhidi ya watani wao wa jadi Simba, ni sehemu ya utimilifu wa kauli hii.
Ni imani yangu kuwa uongozi wa klabu ya Yanga uliangalia uwezo wa kocha huyu hususani kipindi chake alichoinoa Taifa Stars na kujiridhisha kuwa anaweza kuwa mbadala sahihi wa kocha Ernie Brandts ambaye naye alikumbwa na “mafuriko” haya.
Nakumbuka jinsi ambavyo watu walivyofurika katika mitaa ya Twiga na Jangwani wakati wa kumpokea kocha Ernie Brandts, wengine wakianzia uwanja wa ndege wa J.K Nyerere kuonesha shauku yao kwa kocha huyu lakini ilimuwia kusahau mapokezi yote aliyopewa wakati anawasili baada tu ya mabao matatu ya Simba katika mchezo wa nani mtani jembe msimu uliopita. Brandts alifungashiwa akaenda.
Leo tunashuhudia Mbrazil Maximo aliyetua kwa mbwembwe katika kazi yake ya pili ya ualimu Tanzania akiongozana na Wabrazil wenzake Jaja na Coutinho naye anafungashiwa virago ugonjwa ukiwa ni ule ule ulioua kibarua cha Brandts wa mechi dhidi ya Simba.
Kocha wa Yanga, Hans Van Pluijm

Sasa pengo lake limezibwa na kocha aliyewahi kuinoa timu hiyo kabla ya kwenda Uarabuni kuinoa klabu ya Al Shoula, Hans Van Der Plujim.
Misemo ya wahenga bado itatawala ikiwemo huu “mwenzako akinyolewa zako tia maji”. Maneno haya ni vizuri aambiwe kocha Hans kutokana na yeye kurudi kuvaa viatu alivyoaviacha msimu uliopita na hajui kama vitakuwa saizi yake au vitakuwa aidha vikubwa ama vidogo kwake.
Na kama ugonjwa huu wa makocha kupoteza vibarua katika mchezo wa watani wa jadi, bado kuna mchezo wa Simba na Yanga wa ligi kuu katika mzunguko wa pili, je hautakuwa ‘ebola’ kwa kibarua chake?
Sote tunamtakia kila la kheri katika kibarua chake licha kutolewa katika robo fainali ya michuano ya mapinduzi lakini ana kila sababu ya kuliangalia hili.
Inaonekana kutolewa robo fainali mapinduzi si shida, wala sare na Ruvu si tatizo ila mchawi wa ni mechi ya Simba.
Na vilabu vyetu viweke wazi kuwa vinaajiri makocha kwa ajili ya michezo gani kwa sababu, tumeona Maximo ameiongoza Yanga kwenye michezo tisa akishinda mitano(ya mashindano) na kupoteza mitatu ukiwemo wa nani mtani jembe lakini pointi 15 alizovuna Mbrazili huyu zilionekana nyepesi kwenye mzani wa tathmini kuliko 9 alizopoteza ikiwemo pointi 3 za mchezo usio wa kimashindano(nani mtani jembe).
Sasa tujiulize, hata Maximo angeipa ubingwa Yanga na kupoteza mchezo dhidi ya Simba tu, pia angefungashiwa virago?
Ni kweli David Moyes alitimuliwa kutokana na kupoteza mchezo dhidi ya Manchester City? Mbona Mourinho hakutimuliwa wakati anatandikwa goli tano pale Camp Nou akiwa na Real Mdrid? Au mbona hatukuona kutimuliwa kwa Diego Simeone baada ya kupoteza kwa mabao 4-1 katika mchezo wa fainali wa ligi ya mabingwa dhidi ya wapinzani wao wa jadi Real Madrid kule Estadio  Da Luiz msimu uliopita?
Au kuna vipengele vya kimkataba wanavyosaini makocha hawa juu ya mchezo wa Simba na Yanga? Kunaweza kukawa na maswali mengi juu ya hili lakini bado kuna sababu ya jitihada za makusudi za kulinusuru soka la nchi yetu kwa kutafuta tiba ya’ugonjwa huu.

No comments:

Post a Comment